Isaiah 51:1-7

Wokovu Wa Milele Kwa Sayuni

1 a“Nisikilizeni, ninyi mnaofuatia haki
na mnaomtafuta Bwana:
Tazameni mwamba ambako mlichongwa,
na mahali pa kuvunjia mawe ambako mlichimbwa;
2 bmwangalieni Abrahamu, baba yenu,
na Sara, ambaye aliwazaa.
Wakati nilipomwita alikuwa mmoja tu,
nami nikambariki na kumfanya kuwa wengi.
3 cHakika Bwana ataifariji Sayuni,
naye atayaangalia kwa huruma magofu yake yote;
atayafanya majangwa yake yawe kama Edeni,
nazo sehemu zake zisizolimika ziwe kama bustani ya Bwana.
Shangwe na furaha zitakuwako ndani yake,
shukrani na sauti za kuimba.

4 d“Nisikilizeni, watu wangu;
nisikieni, taifa langu:
Sheria itatoka kwangu;
haki yangu itakuwa nuru kwa mataifa.
5 eHaki yangu inakaribia mbio,
wokovu wangu unakuja,
nao mkono wangu utaleta hukumu kwa mataifa.
Visiwa vitanitegemea
na kungojea mkono wangu kwa matumaini.
6 fInueni macho yenu mbinguni,
mkaitazame dunia chini;
mbingu zitatoweka kama moshi,
dunia itachakaa kama vazi,
na wakazi wake kufa kama mainzi.
Bali wokovu wangu utadumu milele,
haki yangu haitakoma kamwe.

7 g“Nisikieni, ninyi mnaojua lililo sawa,
ninyi watu ambao mna sheria yangu mioyoni mwenu:
Msiogope mashutumu ya wanadamu
wala msitiwe hofu na matukano yao.
Copyright information for SwhNEN